Thursday, January 24, 2013

MAONI YA WATOTO KATIKA KATIBA MPYA





Maoni yameandaliwa na Baraza la Watoto la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania



Tarehe: 22 Septemba 2012 na 8 Desemba 2012






Utangulizi
Baraza la watoto ni chombo huru cha uwakilishi wa watoto kilichoundwa hapa nchini mwaka 2002 na watoto wenyewe chini ya usimamizi wa Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii,Jinsia na Watoto kwa kufuata maelekezo yaliyoko kwenye Sera  ya Maendeleo ya mtoto ya mwaka 1996 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2008 . Hadi kufikia  sasa serikali kwa kushirikiana na wahisani imeunda  mabaraza ya wilaya 87 .  Lengo kuu la kuanzisha Baraza la Watoto ni kuhakikisha  kunakuwepo na ulinzi wa haki  za watoto, ufuatiliaji na kutoa taarifa za uvunjwaji wa haki za watoto  nchini na kuhimiza wajibu wa mtoto.
Tunapenda kutoa Shukurani zetu za dhati kwa Mh. Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuteua na kuunda tume ya kukusanya maoni ya Katiba, pia tunaishukuru Tume hii kwa kutupa nafasi ya kutoa maoni.
Tunatambua serikali imekuwa mstari wa mbele katika kufuatilia masuala ya watoto  ikiwemo kuingiza haki za binadamu kwenye katiba mwaka 1984 na kuanzisha sheria ya mtoto mwaka 2009,  sheria  na sera mbali mbali zinazowagusa watoto.

MAMBO MUHIMU AMBAYO WATOTO TUNAHITAJI YAWEMO KATIKA KATIBA MPYA.
1.HAKI NA WAJIBU WA MTOTO KUWEKWA KATIKA KATIBA
Katiba iliyopo haija onyesha wazi kuhusu upatikanaji wa haki za watoto, kwani katika sura ya kwanza sehemu ya tatu imezungumzia kwa ujumla kuhusu haki za binadamu. Kwa vile watoto ni zaidi 50% ya idadi ya Watanzania na wana mahitaji mengi ambayo yanatakiwa kupewa kipaumbele na taifa, hivyo tunaomba katiba mpya iweke kipengele kinachotamka wazi hasa katika nguzo kuu muhimu za haki za mtoto ambazo ni:

§  HAKI YA KUISHI, Katiba itamke kuwa mtoto ana haki ya kupata chakula, matibabu, mavazi na kuishi kwenye mazingira safi,

§  HAKI YA KULINDWA, Katiba itamke wazi kwamba mtoto ana haki ya kulindwa na taasisi, mtu, jamii, familia na serikali dhidi ya matendo ya ubakaji, udhalilishaji, ukatili, ndoa za mapema, utumikishwaji katika kazi hatarishi,  mimba za utotoni, ukeketaji, kutoa mimba, matumizi ya dawa za kulevya, kuuzwa, kukoseshwa au kupoteza uraia,  vitendo vya ulawiti, kudhulumiwa mali, kutupwa au kutelekezwa na wazazi, kushirikishwa kwenye biashara ya ngono, kuonyeshwa picha za ngono,  mikataba - anapopewa ajira ambazo sio hatarishi mfano anaposhiriki kwenye matangazo yanayolenga kuelimisha jamii, kulindwa dhidi ya matangazo au habari za kutisha mfano picha za maiti na matangazo ya biashara yahusuyo ngono, mtoto alindwe na adhabu kali zinatolewa na jamii, familia na taasisi ambazo  zinapelekea kudhalilisha utu wake na kuhatarisha maisha yake. Mfano watoto kupewa adhabu ya kuchomwa moto, viboko, matumizi ya lugha chafu  zinazowadhalilisha watoto.

§  HAKI YA KUSHIRIKI, Katiba itamke kuwa mtoto ana haki ya kushiriki kikamilifukatika kutoa mawazo au maoni katika mambo yanayohusu maisha yake au jamii na kulenga kuendeleza maisha yake. Pia katiba iweke msisitizo kuwa mawazo ya mtoto yaheshimiwe na yapewe uzito kulingana na upeo,umri na aina ya masuala anayoshirikishwa.

Katiba iweke msisitizo kuwa ushiriki wa mtoto uanzie ngazi ya familia, na maamuzi yote yanatolewa kwenye ngazi hii yalenge au yazingatie maslahi ya mtoto yaani yawe ya manufaa kwa mtoto. Katika hii haki ya kushiriki katiba itoe maelekezo kwa serikali kuweka mfumo ambao utamsaidia ushirikishwaji wa mtoto kwa kuanzisha mabaraza na mabunge ya watoto kuanzia ngazi ya kijiji hadi taifa.

§  HAKI YA KUENDELEZWA, Katiba itamke kuwa mtoto ana haki ya kuendelezwa kimwili, kiakili, kiroho, kimaadili na kijamii. Katiba itamke kuwa mtoto ana haki ya kupata elimu kuanzia ngazi ya awali hadi elimu ya juu, na itoe tamko kwa wizara husika kuweka mazingira bora yatakayomsaidia mtoto kusoma vizuri mfano vifaa vya kufundishia vya kutosha, walimu wa kutosha wenye ujuzi na upatikanaji wa chakula mashuleni

Katiba ionyeshe maadili ya mtoto na mtu mzima kuanzia miaka 18, mfano upendo, kudumisha amani, heshima, adabu umoja na ari ya kujitegemea na kuthamini kazi. Katiba ianishe adhabu zitakazotolewa kwa mtu yeyote atakayeenda kinyume na hayo maadili mfano kuvaa mavazi ya nusu uchi na kutamka matusi hadharani.

§  Haki ya Kutobaguliwa: Katiba itamke kuwa mtoto ana haki ya kutobaguliwa kwa hali yoyote ile mfano kijinsi, hali ya kimaisha , ugonjwa, ulemavu, uyatima na jinsi anayvoonekana mbele za watu, dini, utaifa na utamaduni. Katiba iweke msisitizo kuwa watoto wanapokuwa wanapewa huduma ikiwemo ya elimu, afya,chakula na huduma zozote zile ambazo ni muhimu wanatakiwa wasibaguliwe.

Pamoja na haki nyingine zilizotajwa hapo katiba itamke pia na kuweka msisitizo kuwa mtoto ana haki ya kupata jina zuri kutoka kwa wazazi wake lisilolenga kumdhoofisha mtoto, pia itoe uhuru wa mtoto kubadili jina linalomdhoofisha na kusikia aibu ndani ya jamii.  Pia katiba itamke kuwa mtoto ana haki ya kupata  cheti cha kuzaliwa na kusajiliwa mara tu anapozaliwa

2. WAJIBU WA MTOTO
Mtoto ana haki pia ana wajibu, Katiba itamke wajibu wa mtoto kama ulivyoanisha kwenye sheria ya mtoto ya mwaka 2009, kuwa ni
·         Kufanya  Kazi kwa lengo la kuhimarisha umoja wa familia
·         Kuheshimu wazazi, walezi, wakubwa zake na wazee na kuwasaidia pale wanapohitaji msaada
·         Kusadia jamii na taifa lake kwa kutumia uwezo wake wote wa kimwili na kiakili kulingana na umri wake
·         Kutunza na kuhifadhi mila na desturi sahihi za jamii na taifa lake kama ilivyo kwa watanzania wengine.

Katiba itamke kuwa mtoto atakiwi kuvunjiwa haki yake kwa vile anatimiza wajibu ulioainishwa hapo juu.


        3. HAKI ZA WATOTO  WENYE ULEMAVU
Serikali itambue kuwa ulemavu unatofautiana, kwa hiyo na huduma zinazotolewa kwa makundi haya zitofautiane. Hivyo katiba itamke kuwa watoto wenye ulemavu wana haki za msingi kama watoto wengine mfano haki ya Kupata elimu, matibabu, mavazi, malazi,kushiriki, kupata jina zuri, chakula na ulinzi.

Katiba iweke msisistizo na kutamka kuwa watoto wenye ulemavu wa ngozi wanastahili kupata ulinzi maalumu, kuwa na shule maalumu ambazo ni za bweni na wanapokwenda kwenye mikusanyiko kama mikutano mikubwa wapewe ulinzi na vyombo vya usalama na pia anapokuwa mmoja mmoja apewe msaidizi. Pia katiba itoe tamko kuwa hawa watoto wenye ulemavu wapewa huduma kama vifaa vya kusomea na mafuta kwa ajili ngozi.
Watoto wenye ulemavu wa viungo wana haki ya kupata viungo bandia, baiskeli, elimu, huduma za afya na kuhakisha majengo yanayotoa huduma muhimu ni rafiki kwa walemavu.

Pia katiba itamke kuwa  watoto wenye ulemavu wa macho, wanahitaji vifaa vya kusomea, maandishi ya nukta nundu, fimbo za kutembelea, walimu wa kutosha wenye utaalamu wa kuwafundisha watoto hao.
Pia katiba izungumzie kuwa watoto wenye ulemavu wa kutosikia wanahitaji  walimu wenye ujuzi katika mafunzo ya lugha za ishara.  

4.MABARAZA YA WATOTO YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KUTAMBULIKA KIKATIBA.
Tunapendekeza katiba mpya iweke kipengele cha kutambua mabaraza ya watoto na kutoa maelekezo kwa serikali kuanzisha mabaraza kuanzia ngazi ya mtaa/ kijiji hadi taifa na kutenga rasilimali za kuendesha mabaraza hayo.  Hii itawapa nafasi watoto kukusanyika mahali pamoja, kushiriki na kutoa maoni juu ya masuala yanayowahusu ambayo ni haki yao kikatiba.

5. WATOTO KUWA  NA MBUNGE WAO WA KUWAWAKILISHA BUNGENI
Kwa kuwa watoto ni zaidi ya nusu ya idadi ya watanzania wote na wana mahitaji mengi yanayohitaji kupewa kipaumbele na taifa. Katiba mpya iweke mfumo wa wawakilishi wa watoto bungeni kwa kutoa nafasi 2 za wabunge mmoja kutoka Zanzibar na mmoja kutoka Tanzania Bara wa kuzungumzia masuala yanayowahusu watoto. Katiba itoe tamko kuwa wabunge hao (2) wateuliwe na Raisi kwa kuwashirikisha watoto wa Baraza la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

6. VYETI VYA KUZALIWA KWA WATOTO.
Kumekuwepo na tatizo kubwa la upatikanaji wa vyeti vya  kuzaliwa , na tatizo hili linatokana na baadhi ya wazazi kushindwa kupata fedha za kulipia gharama zilizowekwa kupata cheti cha kuzaliwa, pia sababu nyingine ni kwamba hizo huduma ziko mbali sana na wananchi  hali ambayo inapelekea usumbufu kwa wazazi kutembea umbali mrefu au kuingia gharama kufuata vyeti hivyo kwenye ofisi ya mkuu wa wilaya.

Hivyo basi tunaomba katiba itamke watoto wote kuanzia umri wa miaka 0-17 badala ya miaka 0 - 5 wapatiwe vyeti bure bila mzazi kulipia gharama yeyote.
Pia tunaomba katiba itamke na kutoa mamlaka kwa vituo vya afya, zahanati na hospitali kutoa vyeti vya kuzaliwa.

7. MFUMO WA ELIMU.
Mfumo wa elimu uliopo sasa unaleta ubaguzi kati ya watoto wanaotoka kwenye familia zenye kipato kizuri na familia duni au maskini. Mfano watoto wanaosoma shule za binafsi au ‘English medium school’ wanafanya vizuri zaidi katika masomo hasa sekondari na wengi wao wanaotoka kwenye familia zenze kipato bora na wale wanaotoka familia duni au maskini wanasoma kwenye shule za kawaida ambapo elimu sio bora. Lugha inayotumika kufundishia ni tofauti, uwezo wa walimu ni tofauti na gharama zinazolipwa kwenye hizo shule ni kubwa ambapo mzazi wa kawaida hawezi kulipia

Kutokana na hali hii tunaomba Katiba itamke kuwa lugha ya kufundishia iwe ya kiingereza katika shule zote kuanzia awali, mitaala yote ya kufundishia iwe sawa na muda wa kubadilishia mtaala uwe mrefu angalau miaka 10 ili tuone matunda ya mitaala hiyo.  katiba itoe tamko kuwepo mfumo maalumu wa kitaifa wa kubadilisha  mitaala na mfumo huo uwashirikishe wadau wa elimu wakati wa kufanya marekebisho kwenye  mitaala.  Pia katiba itamke uwepo wa taasisi au bodi maalumu ya kuratibu gharama za uendeshaji wa shule za sekondari, misingi na elimu ya juu (vyuo vikuu)  

8.MFUMO WA HUDUMA ZA AFYA
Katiba mpya itamke wazi huduma za afya kwa watoto zitolewe bure kuanzia miaka 0 -17, na itoe maelekezo kwa serikali na sekta husika kuweka mifumo ambayo itasaidia huduma hizo kupatikana bure. Mfano  uchangiaji wa bima za afya ngazi ya kaya. Ili kuboresha afya ya mama na mtoto tunaomba katiba itamke kuwa mama anapojifungua apewe likizo ya miezi 6 ili aweze kumunyonyesha mtoto miezi 6 mfululizo bila kumpa chakula  chochote  tofauti na ilivyokuwa awali, hii itasaidia wanawake kupata muda mzuri wa kuwa karibu na kuwanyonyesha watoto wao kwa muda wa kutosha.

9.MASUALA YA MUUNGANO
Suala la elimu ya awali hadi sekondari liwe la muungano, kusiwepo utofauti wa mitaala kati ya Tanzania visiwani na Tanzania bara ili kuweka usawa katika ufahamu na uelewa wa watoto na taifa kwa ujumla.

10.SHERIA , SERA , MILA NA DESTURI ZINAZOVUNJA HAKI ZA WATOTO
Katiba mpya itamke wazi sheria, sera na taasisi zote zinazokiuka na kuvunja haki za watoto zifutwe. Kwa mfano sheria au sera ya elimu inayotamka kumfukuza mtoto wa kike anapopewa mimba wakati akiwa shuleni, imegundulika kwamba watoto wanaoachishwa shule au kufukuzwa shule kwa ajili ya mimba wanaishia mitaani, wengine wanaamua kuolewa wakiwa na umri mdogo mwisho wa siku tutakuwa na taifa lenye watoto wa kike wengi wasiokuwa na mwelekeo wa kimaisha au wasiokuwa na elimu. Kupata mimba kisiwe kigezo cha kumvunjia mtoto haki yake ya kusoma. Kutokana na hili suala tunapendekeza katiba iweke kipengele cha kufuta  sheria ya Elimu inayotamka kuwa mtoto wa kike akipata mimba afukuzwe shule na kurudisha nyumbani pia itoe tamko moja kwa moja kuwa mtoto akipewa mimba arudi shule, katiba itoe maelekezo ya kumrudisha mtoto shule nyingine ili aweze kuendelea na masomo.

Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 inapelekea watoto kuvunja haki zao kwa kuwa inamruhusu mtoto wa kike kuolewa akiwa na umri wa miaka 15 kwa ridhaa ya wazazi na wakiume kuoa akiwa na umri wa miaka 18, kwa kuwa vitendo vya watoto wa kike kuolewa wakiwa wadogo vimekidhiri, taifa halihitaji tena kuwa na sheria hiyo kwani inakinzana na sheria nyingine kama vile sheria ya mtoto ya mwaka 2009  ambayo imeanisha umri wa mtoto na majukumu ya mtoto, pia inatoa ubaguzi na kuonekana inamkandamiza na kumbagua mtoto wa kike kwanini imruhusu mtoto wa kike kuolewa na umri wa miaka 15 na mtoto wa kiume kuoa akiwa na miaka 18. Pia kuendelea kuwepo kwa sheria hiyo kutawapa fursa wazazi kuendelea kuwaozesha mabinti zao badala ya kuwaendeleza kwa vile sheria inawalinda. Hivyo Basi tunapendekeza katiba ije na tamko la kuwa umri wa kuolewa au kuoa ni miaka 18 na itoe tamko la kufutwa sheria ya ndoa kama itakuwa haijabadili kipengele hicho ndani ya mwaka mmoja tangu kutungwa kwa katiba.

Sheria ya Makosa ya Kujamiiana ya mwaka1998, watoto tunatambua kuwa kuna marekebisho madogo yaliyofanywa kwenye sheria hiyo baada ya kutungwa kwa sheria ya mtoto mwaka 2009 hasa kwenye adhabu kwa mtoto aliyefanya kosa la kujamiiana mtoto mwenzake. Ila kipengele kinachotamka kuwa mtu hatahesabika amembaka msichana mwenye umri wa miaka 15 ikiwa amejamiiana naye wakiwa katika ndoa ambayo wazazi wameridhia hakikufanyiwa marekebisho kipengele hiki kinaendelea kulinda kile kipengele kilicho kwenye sheria ya ndoa kinachomruhusu mtoto wa kike mwenye umri wa miaka 15 kuolewa. Tunaomba katiba itamke kufutiliwa mbali kipengele hicho kwani kinaendelea kunyima haki mtoto kwa kumshirikisha kwenye vitendo vya ngono akiwa mdogo.

Sheria na miongozo ya Elimu iliyopo kwa ajili ya matumizi ya adhabu ya viboko mashuleni. Suala adhabu ya viboko mashuleni zimekithiri na walimu wanatoa adhabu ya viboko bila miongozo iliyopo hadi kufikia watoto kuchapwa bila kufahamu kosa lake. Adhabu nyingine mbaya kwa watoto ni pamoja na watoto kuchimba mashimo, kung’oa visiki, kupiga magoti na kufyatua tofali.  Adhabu hizo zinamuathri mtoto kimwili na kisaikolojia   pia kumdhalilisha mtoto ambavyo ni kinyume na haki za mtoto zilizoainishwa kwenye sheria ya mtoto na mikataba ya kimataifa zinazozuia kumjeruhi mtoto kimwili, kumdhalilisha na kufanyiwa vitendo vya ukatili vyenye kumshusha utu na hadhi kwa mtoto. Hivyo tunaomba katiba itoe tamko la kufuta hiyo miongozo na sera hizo kwani zinatoa mwanya mkubwa kwa walimu kuendelea kuwanyanyasa watoto. Pia katiba itoe tamko kwa jamii kuacha mila au utamaduni zinazoleta madhara kwa mtoto, kwa mfano suala la viboko na adhabu kali zimeonekana pia zikitolewa na wanafamilia, na ni utaratibu umekuwepo kizazi hadi kizazi.

11. TUME YA TAIFA YA HAKI ZA WATOTO
Katiba mpya iunde tume huru ya kudumu ya taifa ya haki za mtoto yenye utaalamu wa kushughulikia haki za watoto ikiwa ni pamoja na kusimamia, kupokea taarifa,  kufuatilia uvunjwaji na kutoa mapendekezo juu ya hatua za kuchuliwa na serikali au taasisi dhidi ya ukiukwaji wa haki za mtoto. Pia itoe maelekezo ya uundwaji wa kamati mbali mbali zinazoshughulikia masuala ya watoto kuanzia ngazi ya mtaa/ kijiji hadi mkoa zitakazo fanya kazi kwa karibu na tume.

12.ULINZI WA WATOTO AMBAO HAWANA MAKAZI MAALUMU,NA WALE WAISHIO KATIKA MAZINGIRA HATARISHI.
Katiba itoe tamko kuhusu utekelezwaji  wa mifumo ya ulinzi wa mtoto iliyoko nchini mfano ule mpango mkakati wa ulinzi wa mtoto kuanzia ngazi ya kijiji hadi taifa ya kushughulikia masuala ya watoto  waishio katika mazingira hatarishi au maelekezo  kwa serikali na sekta husika kuweka mfumo maalumu juu ya ulinzi wa watoto ambao hawana makazi maalumu na waishio katika mazingira hatarishi.

13.KUWEPO NA WIZARA YA WATOTO TU.
Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto inayoshughulikia masuala ya watoto hivi sasa imeelemewa na mambo mengi na hata bajeti inayotengewa kwa ajili ya wizara hiyo haikidhi mahitaji ya watoto. Hivyo tunapendekeza katiba mpya ije na tamko la kuunda wizara maalumu kwa ajili ya watoto kwani vile watoto ni sehemu kubwa sana ya watanzania wote kwani zaidi ya nusu ya watanzania ni watoto kwanini tuchanganywe na na wizara zingine?

HITIMISHO
Baraza la watoto linaahidi kushirikiana na tume katika mchakato mzima wa upatikanaji wa katiba mpya.

No comments:

Post a Comment